
Posted on 30 June 2011
BENDI ya muziki wa dansi yenye maskani yake jijini Dar es Salaam ya Extra Bongo”Next Level” imesema imemuongeza mwimbaji na mtunzi mahiri wa muziki huo, Ramadhani Massanja maarufu kama Banza stone katika kikosi chake kutokana na kuwa na uwezo mkubwa kimuziki.
Alisema kutokana na hilo bendi yake ikafikia uamuzi wa kumchukua mwimbaji huyo kwa nia ya kuongeza nguvu kwa bendi hiyo ili kuweza kujiongezea washabiki.
“Banza ni mwanamuziki mwenye uwezo na kipaji kikubwa katika muziki,hii ndiyo sababu kubwa ambayo imetupelekea kumchukua katika bendi hii, Banza amekuja na sasa tupo studio kwa ajili ya kurekodi vibao kadhaa vikiwemo “Ufisadi wa Mapenzi”, kilichotungwa na Roggary Hegga “Katapila” na “Neema” kilichotungwa na Athanas Mantabe na hapo badaye tutarekodi cha Banza, kilichobeba jina la “Watu na Falsafa ya Maisha” alisema Choki.
Choki alisema kibao chao kipya,ambacho kinasikika katika vituo vya redio, “Mtenda Akitendewa” kimeonyesha mafanikio makubwa kwa washabiki wa muziki, hali inayowapa nguvu kurekodi vibao vingine kwa sasa.
Kiongozi huyo aliwataka washabiki wa bendi hiyo kujitokeza kwa wingi katika maonyesha yao ambayo siku ya alhamis yanafanyika katika ukumbi wa Mzalendo Pub, Kijitonyama, ambapo wasichana huingia bure siku hiyo.
Ijumaa bendi hiyo hutoa burudani katika ukumbi wa Meeda ulipo Sinza na jumamosi bendi hiyo hutoa burudani zake katika ukumbi wa Star Coco Club (Coco Beach)
Source: BurudaniKilaSiku