
Posted on 05 January 2012
MSANII mwenye uwezo wa kuzungumza sauti za viongozi bongo, Steve Nyerere, amezungumza na DarTalk na kusema kuwa anatarajia kwenda Butiama kwa ajili ya kutengeneza filamu yake mpya inayokwenda kwa jina la ‘Respect Nyerere’.
Kabla hajazungumzia ujio wa filamu hiyo Steve, alisema hivi sasa kazi zake zitakuwa tofauti na wasanii wengine kwani hawezi kucheza filamu za mapenzi, badala yake anajikita katika Siasa pekee.
Alisema filamu hiyo ya ‘Respect Nyerere’, itakuwa inahusu mambo yote aliyoyafanya baba huyo wa taifa, kama vile kukemea rushwa, viongozi wabovu, migomo ya wanafunzi na wafanyakazi, ukabila na udini na mambo mengine ambayo yalikuwa na lengo la kuleta maaendeleo ya taifa.
“Sasa ni wakati wa kuwaonesha Watanzania mambo ambayo yalipaswa kufanyiwa kazi na viongozi wetu wa sasa, ambayo baba wa taifa Mwalimu Nyerere aliyafanya, yapo mengi ambayo yanapuuzwa na viongozi wetu kwa manufaa yao binafsi,” alisema.

Steve Nyerere akiwa kwenye pozi la picha na Mh. Rais Jakaya Mrisho Kikwete
Pia alisema kuwa baada ya kazi hiyo kukamilika atakuwa katika maandalizi mengine ya kutoa filamu ya inayokwenda kwanda kwa jina la ‘I love you Zanzibar’, ambayo itakuwa mahususi kwa watu wa visiwani humo.
Alisema kazi hiyo itaelezea pia mambo yetu ambayo yanapatikana katika visiwa hivyo pamoja na siasa zake ambazo zilizungumzwa na viongozi waliyowahi kutawala visiwa hivyo.