
Posted on 10 July 2012
BAADA ya kufanya vizuri na ngoma yake ya ‘Nunda’, msanii mkongwe ndani ya muziki Banana Zorro, amesema kuwa tayari ameshakamilisha kibao kingine kinachokwenda kwa jina la ‘Jirani’, ngoma ambayo kwa sasa ipo kwenye mchakato wa kutolewa video.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, msanii huyo anayetokea kwenye familia ya kimuziki, alisema kuwa audio ya ngoma hiyo bado hajaiachia kwani anakamilisha video ili aweze kuzitoa zote kwa pamoja.
“Baada ya ngoma yangu ya Nunda, kufanya vilivyo kwenye soko sasa nipo katika harakati za kumalizia kitu kipya ambacho naamini kitakuja kuteka soko, hivyo nawaomba mashabiki wa kazi zangu wasubili ujio huo,” alisema.
Hata hivyo aliongeza kuwa katika kuwapa zaidi burudani mashabiki wa bendi yake ya B-Band, inapiga kwenye ukumbi wa Q-Bar Oysterbay kila siku Alhamisi, ambapo anaamini katika burudani hiyo mashabiki wake wataweza kupata ladha ya nyimbo zake zote zilizowahi kutamba na zinazotamba kwa sasa.